Wagonjwa Nane wa Moyo, Wapandikiziwa Betri

Health and Relationships / 26th October, 2022

Mkurugenzi mtendaji Hospitali ya Benjamini Mkapa Dkt. Alphonce Chandika, amesema kuwa hospitali hiyo imefanikiwa kutoa huduma ya kupandikiza betri kwenye moyo kwa wagonjwa nane, ambao mpaka hivi sasa wanaendelea na majukumu yao kama kawaida.


Dkt. Chandika amesema hayo leo Oktoba 26, 2022 Jijini Dodoma, wakati akizungumza na waandishi wa habari akieleza kuhusu utekelezaji wa shughuli mbalimbali za hospitali na utekelezaji wa bajeti kwa mwaka wa fedha wa 2022-2023.


 "Kuna wagonjwa nane ambao mapigo yao ya moyo yanashuka sana, walihudumiwa katika Hospitali ya Benjamin Mkapa kwa kupandikizwa betri kwenye moyo na kupitia maabara hiyo tumeweza kuhudumia watoto 14 waliozaliwa na matatizo ya moyo,"Amesema Dkt.Chandika


Hata hivyo Hospitali imeanza kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto wenye matatito ya kuzaliwa ya moyo, ambapo mpaka hivi sasa tayari watoto kumi wametibiwa.


Aidha, amesema kuwa wagonjwa 39 waliobainika kuwa na matatizo makubwa ya moyo wamehudumiwa kwa kuwekewa vipandikizi, huku wagonjwa wawili kati yao wamehudumiwa kwa dharura ambapo kama ingekuwa ni kusafirishwa kwenda kupatiwa matibabu Dar es Salaam wangepoteza maisha.


Pia tangu mwaka 2020, Hospitali ilifanikiwa kuanzisha upasuaji wa nyonga na magoti kwa kuweka vipandikizi, hadi sasa jumla ya wagonjwa 56 wamewekewa vipandikizi hivyo kwa wastani wa gharama ya shilingi milioni 12. Gharama za huduma hii nchi za nje ni takriban milioni 35 ambapo kwa wagonjwa 56 waliohudumiwa , Serikali imeokoa jumla ya Shilingi bilioni 1.28


"Hospitali hii ndio pekee nchini imefanikiwa kuanzisha huduma ya uvunjaji wa mawe kwenye figo kwa kutumia mawimbi na miale pasipo kumfanyia mgonjwa upasuaji, huduma hii imeshatolewa kwa wagonjwa 148 kwa gharama ya Shilingi milioni 1.2 kwa mgonjwa mmoja, kwa nje ya nchi gharama ni zaidi ya milioni 7 ambapo kwa wagonjwa 148, Serikali imeokoa zaidi ya Shilingi milioni 850,"Ameeleza Dkt.Chandika


Katika hatua nyingine, hospitali ya Benjamini Mkapa imezindua mtambo wa kuzalisha hewa  tiba ya 'Oxygen' katika ambapo imesaidia kuokao zaidi ya milioni 500 na kuongeza mapato ya ndani ya Hospitali kwa kukusanya zaidi ya Shilingi milioni 75 ambazo Hospitali zingine zinachangia kwa kupelekewa huduma hiyo.


Mtambo huo una uwezo wa kuzalisha mitungi 400 ndani ya masaa 24, tangu mtambo huu uzinduliwe, Julai 1, 2022, jumla ya mitungi 13,467 imeshazalishwa ambapo mitungi 10,962 imetumiwa hospitali hapo na mitungi 2,505 ilisambazwa kwenye Hospitali zenye mahitaji.