Udumavu 37.2%, Watoto chini ya Miaka mitano Dodoma

Health and Relationships / 18th October, 2022

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema kwa mwaka 2018 tafiti zimeonesha kuwa kiwango cha Udumavu kwa watoto wenye umri wa miaka mitano katika mkoa wa Dodoma ni 37.2%, huku watoto  wenye upungufu wa uzito wakiwa ni 17.8% na Ukondefu 3.7%.


Senyamule ameyasema hayo leo Oktoba 18, 2022, Jijini Dodoma wakati wa zoezi la utiaji saini mikataba ya utendaji kazi wa shughuli za lishe kati ya mkuu wa mkoa na wakuu wa wilaya.


“Naona utapiamlo bado upo lakini pia udumavu ni  kiashiria kimoja kikubwa sana cha kuonesha bado tunalo tatizo, japokuwa tuliomba watu wafanye tafiti tujue angalau hali ilivyo kwasasa au kama kuna mabadiliko kwani takwimu tulizonazo ni zile za mwaka 2018” Amesema Senyamule.


Katika hatua nyingine, Kaimu Afisa Lishe mkoa wa Dodoma, Adella Mlingi amesema kuwa mikataba hiyo inalengo la kuboresha hali ya lishe na utapiamlo katika mikoa na halmashauri, kusimamia ipasavyo utekelezaji wa afua za lishe ili kupunguza athari za udumavu na utapiamlo kwa watoto chini ya miaka mitano pamoja na kupanga, kutenga na kutoa fedha zote kwaajili ya kutekeleza afua za lishe katika mipango ya Halmashauri kwa mujibu wa miongozo iliyopo.


“Kwahiyo kwa kuingia mkataba huu, tunahakikisha kwamba halmashauri zinaweza kutekeleza afua za liche nchini, ili mwisho wa siku kupunguza hiki kiwango cha udumavu, kiwango cha watoto wenye uzito pungufu lakini pia ukondefu kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano” Amesema Mlingi.


Itakumbukwa kuwa Septemba 30, 2022, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluh Hassan aliingia mikataba na wakuu wa mikoa nchini, inayohusu masuala ya lish,  itakayokwenda  kutekelezwa  kuanzia ngazi ya kijiji na halmashauri.


Aidha, wito umetolewa kwa wananchi wote kuhakikisha kuwa wanazingatia maelekezo wanayopewa na wataalam wa lishe katika kuhakikisha wanapata lishe bora, lakini pia mama wajawazito wanapaswa kufika mapema katika vituo vya afya, ili kupatiwa huduma mbalimbali na watoto wapatiwe vidonge vya Vitamin A.