Huduma ya Afya Akili Bila Malipo Kuanzia Oktoba 7-10,2022

Huduma ya Afya Akili Bila Malipo Kuanzia Oktoba 7-10,2022

Health and Relationships / 7th October, 2022

Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali ya taifa ya afya ya akili Mirembe  Dkt. Paul Lawala amesema hivi sasa kumekuwepo na matukio mengi yanayotokea kwenye jamii yanayo sababishwa na matatizo ya afya ya akili  hali inayo pelekea kuleta madhara makubwa .

 

Kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Afya Duniani (WHO) ya mwaka 2019, kila sekunde 40, mtu mmoja hupoteza maisha kwa kujiua. 

 

Katika ripoti yake ya mwaka 2022 imewahimiza viongozi na watetezi wa afya ya akili kuongeza nguvu ,kujitolea na kuchukua hatua ili kubadilisha mitazamo,vitendo na mbinu ya kuboresha afya ya akili katika jamii zote, lakini pia kukabiliana na viashiria vyote vya kuondoa unyanyapaa na kusisitiza utunzaji wa afya ya akili.

 

Dkt. Paul ,amezungumza hayo Oktoba 6, 2022 jijini Dodoma wakati akiongea na waandishi wa habari kuelekea kilele cha maadhimisho ya afya ya akili yanayoadhimishwa Oktoba 10 ya kila mwaka.

 

“Tunatambua kuna wingi wa matukio ambayo yapo katika jamii yetu kwa sasa ni matukio ya kutisha pia . Ambayo yanatokea katika familia kwa sasa haiwezi kupita wiki moja haujasikia kwamba kunatukio limetokea kwenye jamii. Matukio ambayo kwa siku za nyuma tulikuwa hatuja yazoea sana. Na kwa vyovyote vile matukio hayo yana sehemu moja wapo kwenye afya ya akili.’’ amesema

 

Kuelekea kilele hicho, amewataka wakazi wa Dodoma na mikoa ya jirani kujitokeza kuadhimisha siku hiyo .

 

‘’Sisi kama hospitali tumepanga na tumeadhimisha kutoa huduma bila malipo, huduma ya afya ya akili kwa umma kuanzia tarehe 7 Oktoba mwaka huu mpaka siku ya kilele tarehe 10 Oktoba.’’ amesema Dkt Lawala

 

Ameongeza kuwa, wanategemea kutoa huduma za uchunguzi wa afya ya akili na huduma ya uchunguzi wa magonjwa mengine ya kimwili ikiwemo shinikizo la damu. 

 

''Pia, uzito wa mwili ,ushauri kuhusu upimaji wa maambukizi ya virusi vya ukimwi VVU, huduma za kisaikolojia pamoja na elimu juu ya magonjwa ya afya ya akili na athari za madawa ya kulevya.'' amesisitiza 

 

Katika hatua nyingime,  ameiomba Serikali kuendelea kuchochea uwekezaji kwenye eneo la afya akili ,hasa kwenye eneo la uboreshaji wa miundombinu ,upatikanaji wa dawa na  vifaa tiba na uwezeshwaji wa mafunzo ya wataalam wa afya ya akili katika ngazi ya ubingwa na  ubingwa bobezi.

 

“Hospitali ina wataalam bingwa wa afya ya akili wa nne tu. Na tunakabiliwa na ukubwa wa huduma na mahitaji kwa maana ya kwamba sasa hospitali hapa tuna wagonjwa waliolazwa 400 .Wagonjwa waliokuja kwaajili ya kupata tiba katika mfumo wa kisheria 250 sehemu ya Isanga . Wagonjwa ambao ni waraibu wa dawa za kulevya 500 sehemu ya Isanga. Na tuna wagonjwa 250 ambao tunawaona kama wagonjwa wa huduma za nje.’’ amesema

 

Kufuatana na taarifa ya Shirika la afya Duniani (WHO) baadhi ya magonjwa ya akili yanaanzia katika umri wa miaka 14 na kuendelea na mengi hayabainiki, jambo ambalo linahatarisha zaidi afya ya akili.