“Sheria ya Kulinda wawekezaji iangaliwe upya” Rais Samia

“Sheria ya Kulinda wawekezaji iangaliwe upya” Rais Samia

Business / 29th September, 2022

DODOMA

Rais Samia Suluh Hassan, amemtaka mwanasheria mkuu wa serikali, kupitia upya sheria ya kulinda uwekezaji, kwani sheria iliyopo ya kutaka migogoro yote baina ya nchi na mwekezaji kutatuliwa ndani ya nchi, imekuwa ikipelekea nchi kukosa wawekezaji wakubwa.


“Kuna mashauri ambayo kweli tunaweza kuyafanya hapa ndani, lakini kwa mwekezaji aliye serious hawezi kukubali, ukimpa kipengele hiki cha sheria anakimbia” amesema Rais Samia.


“Uwekezaji lazima ulindwe, nendeni mkalinde uchumi wa nchi yetu kihaki na kiuwadilifu, ili nchi yetu ipokee wawekezaji wengi Zaidi, tukuze uchumi na maslahi yapatikane  zaidi”.


Rais Samia ameyasema hayo, wakati wa mkutano wa Chama cha Mawakili nchini, uliofanyika leo Septemba 29, 2022 katika ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete Jijini Dodoma, wenye kauli mbiu “Utekelezaji wa Majukumu, unaotekeleza sheria na nyenzo muhimu  kwa maendeleo ya taifa”


Aidha, Samia amesema kutokana na serikali kuifungua nchi kwa kiasi kikubwa, imepelekea ongezeko kubwa la wawekezaji nchini, hivyo mawakili watarajie ongezeko kubwa la migogoro ya kibiashara au inayokinzana na sheria za nchi, hivyo ili kuwe na uwekezaji mzuri wenye kukuza uchumi wan chi, mawakili wametakiwa kuwa makini katika kusikiliza na kutatua migogoro hiyo.


Katika hatua nyingine, Rais Samia amewataka wanasheria wote kuhahikisha wanajisajili, ili waweze kutambulika na serikali.


“Wale ambao bado hawajajisajili wanapaswa kujisajili, vinginevyo baada ya muda kupita hatutawatambua kama mawakili wa serikali, itabidi watafute sekta nje waingie au sijui watafanya utaratibu gani na Mwanasheria mkuu wa serikali ili wajisajili”.


Rais Samia, ametoa wito kwa Wanasheria na Mawakili kutoa elimu kwa wananchi kuhusu sheria hususani zinazowagusa sana wananchi, na taratibu ya jinsi ya kupata haki zao, lengo likiwa ni kupunguza mlundikano wa mashauri ambayo hayana ulazima wa kufikishwa mahakamani kwa utatuzi.


Miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo ni Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbalo, Naibu Mwanasheria Mkuu wa serikali, Dkt Evaristo Longopa, Jaji mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Ibrahim Hamis Juma, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Dkt. Elieza Mbuki Jeleshi, na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule.