TASAC Yafafanua Juu Ya Tuhuma Zinazoendelea kwenye Mitandao

General / 11th March, 2023

Shirika la Wakala wa Meli Tanzania (TASAC) limetoa ufafanuzi kuhusu taarifa inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii hususani Twitter na Instagram yenye malalamiko dhidi ya Shirika hilo kuhusu vijana zaidi ya 400 waliokuwa TASAC wakipata elimu ya mafunzo kwa vitendo (intern)



Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Kaimu Mkeyenge, ametoa taarifa hiyo leo March 10,2023 Jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu taarifa hiyo na kutolea ufafanuzi kwa umma kuhusu vijana hao.



Mkeyenge amesema kuwa tuhuma walizotoa Vijana hao  ni pamoja  na Kuvunjwa kwa mikataba bila kufuata utaratibu, kufanya kazi bila bima ya afya na kwamba TASAC ilitoa rushwa kwa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) katika mashauri ya kazi yaliyofunguliwa na vijana hao ili haki isitendeke.



“Hakuna sheria inayomtaka muajiri yeyote yule kumkatia bima ya afya kijana anayefanya shughuli za Mafunzo kazini suala hilo halipo na hakuna taasisi yeyote inayoweza kufanya hivyo kwani stahiki zao zimeainishwa kwenye Muongozo wa Kitaifa wa Mafunzo Kazi uliotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemav”amesema Mkeyenge 



Aidha, Mkurugenzi huyo amesema kuwa kati ya vijana 209 waliofutiwa mikataba yao, ni vijana 41 tu ambao hawakuridhika na maamuzi hayo ambapo vijana 32 kati ya vijana 41, shauri lao lilifutwa na CMA kwa kuwa liliwasilishwa nje ya muda, hivyo ni vijana 9 tu ambao shauri lao dhidi ya TASAC lilipokelewa na lipo katika Tume ya Usuluhisi na Uamuzi na  vijana 168 waliobaki hawakupinga uamuzi wa TASAC wa kuvunja mikataba yao kutokana na mabadiliko ya Sheria ambayo yalikuwa ni nje ya uwezo wa Shirika.



Amehitimisha ufafanuzi huo kwa kusema kuwa TASAC ni taasisi ya Serikali inayosimamiwa na Sheria, Kanuni na Miongozo ya Serikali, hivyo mashauri yake kisheria yanasimamiwa na Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ikiwa ni pamoja na shauri hilo, hivyo Shirika halijatoa na haliwezi kutoa rushwa yoyote kwa CMA ili kuzuia haki isitendeke kama ilivyoripotiwa katika mitandao ya kijamii