Tanzania Kuunga mkono Mpango wa IMF utekelezaji wa mipango ya maendeleo

Tanzania Kuunga mkono Mpango wa IMF utekelezaji wa mipango ya maendeleo

General / 23rd January, 2023

Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba  amesema kuwa Tanzania inaunga mkono mpango ulioanzishwa na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) kuingiza masuala ya kijinsia kwenye utekelezaji wa mipango yake ya maendeleo.


Dkt. Nchemba ameyasema wakati akifungua mkutano wa majadiliano kuhusu mkakati wa Shirika hilo wa kuingiza masuala ya kijinsia kwenye mipango yake, uliofanyika jijini Dar es Salaam na kuwashirikisha wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi.

Amesema kuwa kwa upande wa Tanzania, Serikali itaendelea kutilia mkazo masuala hayo ya kijinsia kwa kuwekeza rasilimali fedha katika kuboresha afya ya mama na mtoto, utoaji elimu bila ada, na kuwawezesha wanawake kiuchumi.

Aidha Dkt. Nchemba ameiomba jumuiya ya kimataifa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kufanikisha masuala hayo na kusifu ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na IMF ambapo ushirikiano huo umelenga katika maeneo matatu ikiwemo kuelekeza bajeti kubwa kwenye maendeleo ya watu kwa kuboresha makusanyo ya ndani kupitia kodi, kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara na kuimarisha usimamizi na matumizi ya fedha za Umma.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kituo cha Shirika la Fedha la Kimataifa Mashariki (AFRITAC), Bi. Li Xiangming, amesema kuwa Uamuzi wa Shirika lake wa kuingiza masuala ya kijinsia kwenye mipango yake umelenga kujenga jamii yenye usawa na kuwawezesha wanawake kushiriki katika kujenga uchumi na kupata maendeleo endelevu.

Aidha ametaja baadhi ya maeneo yatakayotiliwa mkazo zaidi katika mkakati huo kuwa ni pamoja na kuwawezesha wanawake kiuchumi, kumiliki ardhi, kupata elimu bora na kupiga vita aina zote za ukatili wa kijinsia zinazokwamisha maendeleo ya mwanamke na mtoto.