NMB Yaunga Benki nyingine 17 Kwenye Mtandao Wake wa ATM

NMB Yaunga Benki nyingine 17 Kwenye Mtandao Wake wa ATM

General / 5th March, 2024

Ushirikiano wa Benki ya NMB na UBX inayounganisha Benki 17 kwenye mtandao wake wa Umoja Switch umeiwezesha Benki ya NMB kuunganisha benki hizo 17 kwenye mtandao wake wa mashine za kutolea fedha (yaani ATM interoperability).



Ushirikiano huu unalenga kuongeza wigo wa upatikanaji wa mashine za ATMs na kupunguza gharama za miamala ya ATM kwa wateja wa Benki hizi, na Watanzania kwa ujumla.

Kupitia ushirikiano huu wa Benki ya NMB na UBX, Watanzania watanufaika na mambo yafuatayo:

➡️ Upatikanaji wa Huduma za ATM - Wateja wa Benki zote 17 za Umoja Switch na wateja wa Benki ya NMB watakuwa na uwezo wa kufanya miamala na kupata huduma za kibenki wakati wowote kupitia mtandao wa ATMs zaidi ya 700 za NMB zinazopatikana nchi nzima na ATMs za Umoja Switch (zaidi ya 280) na hivyo kuongeza wigo wa upatikanaji wa huduma.

➡️ Unafuu wa Gharama kwa Wateja - Ushirikiano huu unaongeza ufanisi na kuleta unafuu mkubwa wa gharama za miamala ya ATM. Gharama za miamala ya ATM kwa wateja wa Benki hizi 17 waliokuwa wanatumia ATM za NMB na wateja wa NMB waliokuwa wanatumia ATM za benki hizi zinaenda kupungua kwa zaidi ya asilimia 70%.

➡️ Ujumuishwaji wa Kifedha – Ushirikiano huu utaongeza matumizi ya kadi kwenye ATM nchini na kupunguza foleni matawini – hii ni njia mbadala ya kuongeza ujumuishaji rasmi wa kifedha nchini.

➡️ Ufanisi wa Mabenki - Benki shiriki zitaweza kufikia maeneo yaliyo mbali na ambayo hapo awali ilikuwa vigumu kwa taasisi moja kuyafikia kwa kuweka ATM.

➡️ Unafuu wa Gharama kwa Mabenki - Ushirikiano huu pia, unakwenda kupunguza gharama za uendeshaji kwa benki shiriki. Miamala yote inayofanyika nchini haitakuwa na ulazima tena wa kupitia nje ya nchi, miamala hii itakamilishwa ndani ya mtandao wa NMB na UBX na hivyo kupunguza gharama kubwa za uendeshaji tulizokuwa tukilipa awali, hasa gharama za fedha za kigeni kwa ajili ya kuweka dhamana kwenye taasisi za nje zilizokuwa zinatoa huduma za mtandao kwa ajili ya kukamilisha miamala hii.

Hii ni mara ya kwanza kwa makubaliano ya namna hii kufanyika na hivyo makubaliano haya yanaandika historia mpya katika sekta ya kifedha nchini Tanzania

Akiongea kwenye hafla hiyo Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB - Bi. Ruth Zaipuna alisema: “Nina Imani ya kuwa ushirikiano huu utakuwa mwanzo na chachu ya mashirikiano mengine mengi na ya kimkakati katika sekta yetu ya kibenki nchini Tanzania kwa manufaa ya wateja wetu na Watanzania kwa ujumla. Kupitia mashirikiano ya kimkakati kama haya tutaweza kupiga hatua zaidi katika utoaji wa huduma nafuu, rahisi na salama za kibenki kwa watanzania wote, na hivyo kuchochea ukuaji wa kiuchumi wa mtanzania mmoja mmoja na taifa letu kwa ujumla.”

Mgeni rasmi katika hafla ya uzinduzi huu alikuwa Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb) Naibu Waziri wa Fedha ambaye aliipongeza Benki ya NMB na UBX na kushauri mashirikiano kama haya yaendelee kwa manufaa ya nchi yetu.

Hafla hii ilihudhuriwa pia na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya UBX, ndugu SabaSaba Moshingi na viongozi kutoka mabenki mbalimbali nchini ikiwa ni pamoja na viongozi wa Benki 17 zilizo chini ya Umoja Switch.

Benki zilizo chini ya Umoja Switch ni pamoja na Access Microfinance Bank, Akiba Commercial Bank, Azania Bank, Bank of Africa, DCB Commercial Bank, Letshego Bank, Maendeleo Bank na Mkombozi Commercial Bank. Zingine ni MUCOBA Bank, Mwalimu Commercial Bank, MwangaHakika Bank, Peoples’ Bank of Zanzibar, TCB Bank, Uchumi Commercial Bank, International Commercial Bank na United Bank for Africa.