Makubaliano ya MIF, Equity Bank na Equit Foundation Kusaidia Elimu ya Kifedha kwa sekta mbalimbali

General / 21st November, 2022

Na Rajabu Msangi

Taasisi ya Mwanamke Initiative Foundation, Equity Bank Tanzania pamoja na Equity Group Foundation wameingia makubaliano yanayolenga kuleta maendeleo kwa mtoto wa kike na vijana kwa ujumla.


Hayo yamesemwa leo Novemba 21, 2022 na Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwanamke Initiative Foundation (MIF) ambaye pia ni Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Wanu Hafidh Ameir wakati wa hafla ya utiaji saini wa Makubaliano hayo iliyofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam.


“Mkataba huu utaenda kuiwezesha Taasisi yetu kuleta maendeleo kwa vijana kwa kuongezea ujuzi kupitia VETA, itasaidia katika suala zima la nishati na mazingira kuhakikisha kaya zinapata nishati safi kwa kupikia ili kupunguza uchafuzi wa mazingira” Amesema Mhe. Wanu.


Aidha amesema Makubaliano hayo yatasaidia kutoa elimu kwa wajasiriamali wadogo wakike hasa ya kifedha na jinsi ya kuendesha biashara zao katika kukua na kutengezeza faida.


“Pamoja na hayo, tunaingia makubaliano ya dhamana ya kupunguza hatari yaani ‘risk’ ya mikopo kwa wajasiriamali wadogo na wa kati wengi wamekuwa wakishindwa kulipa mikopo yao, sio kwa sababu biashara ni mbaya bali ni kukosa elimu ya kifedha.


“Katika sekta ya Kilimo, tutahakikisha wakulima wanakuwa katika mfumo rasmi wa kilimo ili waweze kuhudumiwa mahitaji yao na kuongezea mnyororo wa thamani wa bidhaa zao” Ameongeza Mhe. Wanu.


Kwa Upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Equity Group, Dkt. James Mwangi amesema Equit Foundation imekuwa ikitumia njia mbalimbali za kuinua maisha ya watu ikiwemo kuwasaidia watoto yatima kulipa fedha za shule na mahitaji yao muhimu.


“Huo mpangilio sasa tuna watoto 60,000 ambao tumewapatiaufadhili wa masomo ya sekondari halafu tuna watoto 25,000 ambao tumefadhili elimu ya juu yaani ‘University Education’ na 1000 tumewatuma kutafuta ujuzi na elimu katika mataifa mbalimbali” Amesema Dkt. Mwangi.


“Mwaka huu peke yake Equity itatumia Dola za Kimarekani Milioni 60 kulipa gharama za hii mipangilio, kwa hiyo kwa mwaka ujayo tukisema Mwanamke Initiatives atapata nusu ya hizo fedha, watu wengi Tanzania watakuwa wamesaidika, tutafikia wengi, tutaelimisha, tutakuwa na watoto yatima wengi ambao tutakuwa tukilipia ada” Ameongeza Dkt. Mwangi.


Makubaliano hayo yanalenga kuisaidia Taasisi ya Mwanamke Initiative Foundation katika Elimu ya Kifedha na mafunzo ya Ufundi Stadi kwa makundi yanayolengwa kutoka sekta mbalimbali kama vile Kilimo, Afya na Elimu.