Kilele Maadimisho Siku ya Kimataifa ya Usalama na Afya Mahala Pa Kazi Kufanyika Morogoro

Kilele Maadimisho Siku ya Kimataifa ya Usalama na Afya Mahala Pa Kazi Kufanyika Morogoro

General / 27th April, 2023


 


Tanzania inatarajia kuungana na mataifa mengine duniani kuadhimisha siku ya kimataifa ya usalama na afya mahala pa kazi


Hayo yamebainishwa leo April 26, 2023 na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu kazi, Vijana, Ajira na wenye Ulemavu Prof. Joyce Ndalichako wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma.

 


Amesema maadhimisho hayo yameanza rasmi leo yakiambatana na shughuli mbalimbali ikiwemo uhamasishaji, Maonesho na mafunzo ya usalama na afya kwa wafanyakazi, utoaji tuzo  pia yatawakutanisha wamiliki na wasimamizi sehemu za kazi, lengo likiwa ni kutafakari kuhusu usalama wa kazi na kuwakumbuka walioumia au waliopoteza maisha wakiwa katika utekelezaji wa majukumu yao

 


Aidha, ametanabaisha kuwa takwimu za kidunia zilizotolewa na Shirika la Kazi Duniani mwaka 2022 zinaonesha kwamba zaidi ya watu milioni mbili na laki tisa (2.9) hupoteza maisha kutokana na ajali na magonjwa yatokanayo na kazi, Kwa upande wa Tanzania jumla ya ajali na magonjwa yaliyoripotiwa katika Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi kuanzia Julai 2019 hadi Juni 2021 ni ajali 4,993 na magonjwa 249 katika ajali hizo, vifo vilikuwa 217.





Aidha, Prof. Ndalichako amewataka waajiri, wafanyakazi na wananchi wote kwa ujumla kushiriki katika maadhimisho hayo ambayo kitaifa yatafanyika April 28, 2023 mkoani Morogoro, yakiongozwa na Kaulimbiu “Mazingira Salama na Afya Kazini ni Kanuni na Haki ya Msingi Mahala pa kazi”, kaulimbiu inayotokana  na Azimio la Wanachama wa Shirika la kazi Duniani (ILO) katika kikao cha Juni 2022 kilichofanyika huko Geneva Uswisi, na kuamua kuwa suala Usalama na Afya mahali pa kazi liwe mojawapo ya Kanuni na Haki tano za msingi kwa wafanyakazi mahali pa kazi,"

 


Nae Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda amesema kuwa  ajali nyingi zinaripotiwa ni katika sekta ya Uzalishaji ambapo imeajiri vijana wengi huku wengine wakiwa hawana ujuzi wa kutosha katika nafasi wanazofanyia kazi.




"Uzalishaji lina matukio mengi ya ajali na hii ni kutokana na vijana wengi kujikita katika eneo hilo kujiajiri ama kuajiriwa huku wengine wakifanya tu bila kuwa na ujuzi wa kutosha au taaluma kwani eneo hilo mara nyingi wanaangalia nguvu sana kuliko taaluma ndio maana ajali zinakuwa nyingi," amesema Bi.Mwenda

 


Siku ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi Duniani ilianza mwaka1996 Nchini Marekekani Katika Jiji la New York, ambapo waathirika wa watu walioumia na kupoteza maisha wakiwa kazini hukumbukwa. Maadhimisho hayo yalikuwa yakifanywa na Chama Cha Wafanyakazi Duniani. Ilipofika mwaka 2001,Shirika la Kazi Duniani liliona kuwa ni busara kubadilisha madhumuni ya siku hiyo na kuiita “Siku ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi Duniani”.