"Tumeongeza Bil.84" HESLB
Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Tanzania (HESLB)
imethibitisha ongezeko la bajeti ya mikopo kwa mwaka wa masomo 2022/2023 kwa
asilimia 14.7 ikilinganishwa na kiasi kilichotengwa awali.
Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Abdul-Razaq Badru
amesema kutokana na ongezeko hilo la fedha kwa sasa bajeti ya mikopo imefikia
Sh654 bilioni kutoka Sh570 bilioni iliyotengwa hapo awali.
Kiasi hicho kitawezesha wanafunzi 28,000 kupata
mikopo kwa robo ya kwanza ya mwaka wa masomo na tayari fedha hizo
zimeshafikishwa katika vyuo husika.
Hadi kufikia leo jumla ya wanafunzi 166,438
wamepangiwa mikopo yenye thamani ya Sh424.5 bilioni kati yao wa mwaka wa kwanza
ni 68,460 na wanaoendelea ni 97,978.
Kulingana na Badru wanafunzi wa mwaka wa kwanza
wanaolengwa kunufaika na mikopo hiyo kwa mwaka huu ni 71,000.
“Bajeti isingeongezwa ni wazi wanafunzi 28,000
wangekosa mikopo lakini kutokana na hatua hii iliyochukuliwa wataweza kupata
ufadhili huu. Hawa waliopata walikuwa tayari wameshafanyiwa tathmini na
kuonekana mahitaji yao ni makubwa,”amesema Badru.
Itakumbukwa
kuwa hivi karibuni, Spika wa Bunge Dkt. Tulia Ackson aliiagiza Bodi ya Mikopo
ya Elimu ya Juu (HESLB) kufika mbele ya Kamati ya kudumu ya Bunge ya Maendeleo
ya Jamii ili kueleza sababu za kutoipa ushirikiano kamati ya Serikali
iliyoundwa kuchunguza utaratibu wa kutoa mikopo kwa miaka mitano iliyopita.
Alisema
kuhusu hoja kama HESLB inatoa mikopo sawa sawa itajadiliwa Februari mwakani
wakati kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii itakapokuwa inatoa
taarifa yake bungeni na hivyo kuona kama kuna haja ya Bunge kuunda tume ya kuchunguza
bodi hiyo ama la.
Aidha, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya
Jamii, Stanslaus Nyongo alisema Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, (HESLB),
inahitaji Sh800 bilioni ili iweze kutoa mikopo kwa wanafunzi wote waliodahiliwa
kujiunga na vyuo vikuu.