Trilioni 1.49 zatekeleza miradi ya maendeleo TAMISEMI

Trilioni 1.49 zatekeleza miradi ya maendeleo TAMISEMI

General / 2nd March, 2022

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Innocent Bashungwa amesema Serikali ya Awamu ya Sita kwa kipindi cha mwaka mmoja wa uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, Ofisi ya Rais- TAMISEMI imepokea jumla ya Shilingi trilioni 1.49 kwa ajili utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Sekta ya Elimu, Afya na Barabara.

 

Waziri Bashungwa ameyasema hayo leo Machi 01, 2021 wakati akieleza mafanikio ya mwaka mmoja wa Serikali ya awamu ya sita kwenye kikao kazi cha Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakurugenzi wa halmashauri, wakuu wa idara na waandishi wa habari.

 

Amesema katika Sekta ya elimu kiasi cha shilingi bilioni 662.32 zimetumika kujenga shule mpya 257 za sekondari na shule 9 za msingi,kujenga vyumba vya madarasa 18,219 kwa shule za msingi; Vituo Shikizi na Shule za Sekondari; ukamilishaji wa ujenzi wa vyumba vya madarasa 4,525 kwa shule za msingi na sekondari, ukamilishaji wa ujenzi wa vyumba vya maabara 1,399 na matundu ya vyoo 568 kwa shule za msingi na sekondari.

 



Waziri Bashungwa ameendelea kusema kuwa fedha hizo zimeweza ukamilishaji wa mabweni 170 , nyumba za waalimu 42, kwa shule za msingi na sekondari, ujenzi wa Maabara 11 kwa shule za sekondari, Mabwalo 6 kwa shule za sekondari, majengo ya utawala 4 kwa shule za sekondari na ukamilishaji wa Shule Kongwe nne (04) shule za msingi na sekondari.

 

Aidha, Amesema katika Sekta ya Afya serikali ilitoa kiasi cha shilingi bilioni 234.41 kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya 288, Ujenzi wa Hospitali Mpya 28, Ujenzi wa majengo ya Wagonjwa Mahututi 26, Ujenzi majengo ya Dharura 80, ujenzi wa Kituo kimoja cha Matibabu ya Magonjwa ya Milipuko, ujenzi wa Nyumba 150 za watumishi katika maeneo ya pembezoni, ukamilishaji wa Ujenzi wa Zahanati 615, Hospitali 68 za Halmashauri zilizoanza kujengwa Mwaka wa fedha 2018/19, ujenzi wa Hospitali 31 za Halmashaurii na Ununuzi wa Vifaa na Vifaa Tiba kwa Hospitali 31.



 

Vile vile, Waziri Bashungwa amesema katika sekta barabara Shilingi bilioni 597 zimetolewa kwa ajili ya ujenzi, matengenezo na ukarabati wa barabara za Wilaya zinazosimamiwa na TARURA, ambazo zimetumika katika ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami zenye urefu wa kilomita 213.36, Ujenzi wa barabara kwa kiwango cha changarawe zenye urefu wa kilomita 1,152.33, Matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilomita 25,059.4, Ujenzi wa madaraja 201 ambapo ujenzi unaendelea,Ujenzi wa maboksi kalavati 70 na Ujenzi wa mifereji ya maji ya mvua yenye urefu wa kilomita 123.05.