TBS yatakiwa kushiriki utayarishaji viwango vya kimataifa

TBS yatakiwa kushiriki utayarishaji viwango vya kimataifa

General / 18th November, 2022

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara Dkt. Hashil Twalib Abdallah ametaka Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kushiriki kikamilifu katika utayarishaji wa Viwango vya Kimataifa.


Dkt. Abdallah ameyasema leo 18 Novemba, 2022 alipomwakilisha Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara Dkt. Ashatu Kijaji katika kufunga maadhimisho ya Siku ya Viwango Duniani, kufungua Mashindano ya insha na kufungua warsha ya wadau katika uandaaji wa Viwango.

Dkt. Abdallah amelitaka Shirika la TBS pamoja na wadau wa uandaaji viwango wametakiwa kuongeza juhudi katika kuoanisha viwango vyetu katika ngazi za kikanda na pia kushiriki kikamilifu katika michakato ya kutayarisha viwango vya kimataifa ili kuwezesha bidhaa za Tanzania kupenya kirahisi katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Hatua hii imewawezesha kuzalisha bidhaa bora zenye kukidhi matakwa ya viwango hatimaye kuwawezesha kupata masoko ya kimataifa.

Aidha amesema kazi inayofanywa na TBS ya kuratibu na kusimamia utayarishaji wa viwango vya kitaifa ni kazi adhimu. Viwango husaidia si tu kufungua mipaka, lakini pia kuhakikisha usalama wa afya na mali, ulinzi wa mazingira na elimu kwa umma.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Dkt. Athuman Ngenya amesema kuwa maadhimisho ya Siku ya Viwango ya kila mwaka yamelenga kuamsha uelewa miongoni mwa wadhibiti ubora, wafanyabiashara, wenye viwanda na walaji kuhusu umuhimu wa viwango kwa maendeleo ya jamii.