Tanzania yapewa msaada wa Euro mil 10 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mitatu ya kimaendeleo.

Tanzania yapewa msaada wa Euro mil 10 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mitatu ya kimaendeleo.

General / 9th August, 2022

Serikali ya Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani imeipatia serikali ya Tanzania msaada wa Jumla ya Euro Mill 10 sawa na Shilingi za Kitanzania Bill 23.7 kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi mitatu.

Hayo yamejiri leo jijini Dar es salaam katika Hafla ya utiaji wa saini wa mkataba wa ushirikiano kati ya serikali hizo mbili kuhusu miradi mitatu ukiwemo mradi Euro Mill 6 kwa ajili ya kukabiliana na migogoro au muingiliano kati ya wanyama na binadamu kwenye maeneo yanayozunguka hifadhi.

Akizungumza katika hafla hiyo ya utiaji wa saini,Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Emmanuel Tutuba amesema miradi mingine ni mradi wa Euro Mill 3 kwa ajili ya kuwezesha upatikanaji wa haki za wanawake na watoto na wa Euro Mill 1 kwa lengo la kuandaa maandiko ya kitaalamu na kufanya tafiti.

Aidha Tutuba amesema mradi wa kuwezesha upatikanaji wa haki za wanawake na watoto utawezesha makundi maalum kwa kuwa na uwezo wa kudai haki zao na hivyo kupunguza unyanyasaji wa Kijinsia katika maeneo ya utekelezaji wa miradi hiyo.

‘Kuhusu fedha za mradi wa kuandaa maandiko ya kitaalamu na kufanya tafiti zitawezesha kufanya pembuzi yakinifu kwa miradi mbalimbali itakayoiwezesha serikali kupata misaada kwa siku za usoni kupitia Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani’amesema Tutuba

Amesema kuwa msaada huo ni sehemu ya ahadi ya misaada ya jumla ya Euro milioni 71 sawa na shilingi bilioni 188.65 iliyotolewa na Shirikisho hilo, katika majadiliano yaliyofanyika baina ya pande hizo mbili, jijini Dar es Salaam tarehe 25 Novemba 2021 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimaendeleo.


Kwa upande wake Balozi wa Serikali ya Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani nchini Tanzania Regine Hess amesema wataendelea kushirikiana na Tanzania katika kusaidia kufanikisha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimaendeleo.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Khatibu Kazungu ameipongeza serikali ya Ujerumani kwa msaada huo kwani utakwenda kusaidia kupunguza kesi za ukatili wa kijinsia kwa kina mama wazee na watoto nchini.

Naye Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Juma Mkomi amesema msaada huo umekuja muda muafaka kwani utasaidia kukabiliana na changamoto zinazojitokeza baina ya binadamu na wanyama huku pia akiwataka wananchi kuepuka kuingia katika maeneo yaliyohifadhiwa.

Hata hivyo Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Emmanuel Tutuba amemuhakikishia Balozi wa Ujerumani kuwa serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan itaendelea kutekeleza miradi hiyo na fedha zote kuelekezwa katika maeneo yaliyokusudiwa.

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Emmanuel Tutuba (kushoto) na Balozi wa Serikali ya Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani nchini Tanzania Regine Hess (kushoto) wakitia saini ya mkataba wa msaada Euro Mill 10 kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi mitatu.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Emmanuel Tutuba (kushoto) na Balozi wa Serikali ya Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani nchini Tanzania Regine Hess (kushoto) wakibadilishana hati ya mkataba wa msaada waliosaini kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi mitatu.Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Emmanuel Tutuba akizungumza baada utiaji wa saini ya mkataba wa msaada Euro Mill 10 kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi mitatu.Balozi wa Serikali ya Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani nchini Tanzania Regine Hess akizungumza baada utiaji wa saini ya mkataba wa msaada Euro Mill 10 kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi mitatu.