Rais Samia atoa msamaha kwa wafungwa 3,826

Rais Samia atoa msamaha kwa wafungwa 3,826

General / 26th April, 2022


KATIKA kuadhimisha Miaka 58 ya Muungano wa Tanzania Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ametoa msamaha kwa wafungwa 3,826. leo ikiwa ni kuadhimisha miaka 58 ya Muungano wa Tanzania ambao hufanyika kila ifikapo Aprili 26,  kila mwaka. 

Hili ni tukio muhimu na la kihistoria kwa Taifa letu. Katika maadhimisho hayo, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutumia madaraka aliyopewa chini ya Ibara ya 45(1)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ametoa msamaha kwa wafungwa 3,826, Kwa masharti yafuatayo:

(i) Wafungwa wote wapunguziwe robo (1/4) ya vifungo vyao baada ya punguzo la kawaida la moja ya tatu (1/3) linalotolewa chini ya Kifungu cha 49 (1) cha Sheria ya Magereza, Sura ya 58. Wafungwa hao sharti wawe wametumikia robo (1/4) ya vifungo vyao na wawe wameingia gerezani kabla ya tarehe 26 Februari, 2022 isipokuwa wafungwa walioorodheshwa katika sharti la 2(i–ii);

(ii) Wafungwa wagonjwa wenye magonjwa ya kudumu ambao wametumikia
robo (1/4) ya vifungo vyao na wapo kwenye Terminal Stage, ugonjwa huo uthibitishwe na jopo la waganga chini ya uenyekiti wa Mganga Mkuu wa Mkoa/Mganga Mkuu wa Wilaya;

(iii) Wafungwa wazee wenye umri wa miaka sabini (70) au zaidi ambao wametumikia robo (14) ya vifungo vyao. Umri huo uthibitishwe na jopo la waganga chini ya uenyekiti wa Mganga Mkuu wa Mkoa/Mganga Mkuu wa Wilaya;

(iv) Wafungwa wa kike walioingia gerezani wakiwa na watoto wanaonyonya, wasionyonya na wajawazito ambao wametumikia robo (1/4) ya vifungo; (V) Wafungwa wenye ulemavu wa mwili na akili (physical disability and mental disability) ambao wametumikia robo (1/4) ya vifungo vyao. Ulemavu huo uthibitishwe na jopo la waganga chini ya uenyekiti wa Mganga Mkuu wa Mkoa/Mganga Mkuu wa Wilaya;

(vi) Wafungwa waliohukumiwa adhabu ya kuwekwa kizuizini (Under President's Pleasure) ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka kumi (10) na kuendelea;

(vii) Wafungwa waliohukumiwa adhabu ya kifo ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka thelathini (30) na kuendelea;

(viii) Wafungwa wanaotumikia kifungo cha maisha gerezani ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka ishirini (20) na kuendelea;

(ix) Wafungwa wanaotumikia adhabu kwa makosa ya kujaribu kuua (Attempt to Murder) ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka kumi (10) na kuendelea;

(x) Wafungwa wanaotumikia adhabu kwa makosa ya kujaribu kujiua (Attempt Suicide) ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka kumi (10) na kuendelea;

(xi) Wafungwa wanaotumikia adhabu kwa makosa ya kuua watoto wachanga (Infanticide) ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka kumi na tano (15) na kuendelea;

(xii) Wafungwa wanaotumikia adhabu kwa makosa ya uhujumu uchumi ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka ishirini (20) na kuendelea;

(xiii) Wafungwa wanaotumikia adhabu kwa makosa ya matumizi mabaya ya madaraka yao ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka mitano (05) na kuendelea;

(xiv) Wafungwa wanaotumikia adhabu kwa makosa ya utakatishaji wa fedha ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka ishirini (20) na kuendelea;

(xv) Wafungwa wanaotumikia adhabu kwa makosa ya rushwa ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka kumi (10) na kuendelea;

(xvi) Wafungwa wanaotumikia adhabu kwa makosa ya usafirishaji wa madawa ya kulevya ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka ishirini (20) na kuendelea;

(xvii) Wafungwa wanaotumikia adhabu kwa makosa ya utekaji au wizi wa watoto ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka kumi (10) na kuendelea; na

(xviii) Wafungwa wanaotumikia adhabu kwa makosa ya wizi au ubadhirifu wa fedha na mali za umma ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka kumi na tano (15) na kuendelea.

3. Aidha, msamaha huu usiwahusishe wafungwa wafuatao:

(i)Wafungwa wa madeni; na 

(ii)Wafungwa wanaotumikia kifungo chini ya Sheria ya Bodi za Parole, Sura ya 400 Sheria ya Huduma kwa Jamii (Sura ya 291) na Kanuni za Kifungo cha Nje {The Prisons (Extra Mural Penal Employment) Regulations}, 1968.