Kuelekea Uzinduzi wa TTMOA, wataja mafanikio Miradi ya Kimkakati

Kuelekea Uzinduzi wa TTMOA, wataja mafanikio Miradi ya Kimkakati

General / 18th November, 2022

Na Rajabu Msangi


Chama cha Wamiliki wa Matipa na Mashine Tanzania (TTMOA) kimesema kimefanikiwa katika kujumuisha sehemu kubwa ya maudhui ya ndani hasa katika miradi mikubwa na ya kimkakati ya maendeleo ikiwemo kusambaza vifaa na mashine.


Hayo yamebainishwa leo 18 Novemba 2022 na Mwenyekiti wa Chama hicho Emmanuel Moshi wakati akizungumza na waandishi wa habari katika hoteli ya Onomo jijini Dar es Salaam ikiwa ni kuelekea uzinduzi wa Chama hicho cha TTMOA unaotarajiwa kufanyika Novemba 25, 2022.


“Miradi hiyo ni pamoja na Mradi wa Bwawa la Kufua Umeme la Julius Nyerere, Mradi wa Reli ya Kisasa (SGR) kuanzia Dar es Salaam mpaka Mwanza, Miradi mbalimbali ya Mamlaka ya Barabara nchini (TANROAD) tumekuwa tukishiriki moja kwa moja kupeleka vifaa kwa wakandarasi na kwenye sekta ya madini hasa katika makaa ya mawe ambayo ni malighafi inayotafutwa sasa tumeshiriki pia” Amesema Bw. Moshi.


Aidha Bw. Moshi amesema TTMOA ni chama cha biashara ambacho kimeanzishwa tangu mwaka 2018 kikiwa na lengo la kuwawakilisha na kutetea maslahi ya wafanyabiashara wa Tipa na Wamiliki wa Mitambo hapa nchini.


“Lengo ni kupitia sera yenye msingi wa ushahidi, utafiti katika utetezi na ushawishi tukifanya kazi na Serikali kwa niaba ya wanachama wetu” Amesema Bw. Moshi.


 Uzinduzi wa Chama hiki cha Wamiliki wa Matipa na Mashine Tanzania (TTMOA) utafanyika Novemba 25, 2022 katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhe. Atupele Mwakibete kama Mgeni rasmi katika uzinduzi huo.