KNAUF Tanzania Kuwekeza Bilioni 115 upanuzi kiwanda Mkuranga
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Knauf Gypsum Tanzania inajishughulisha na utengenezaji na uuzaji wa vifaa vya ujenzi Ilse Boshoff (kulia) na meneja masoko wa kampuni hiyo Lilian Mangaru (kushoto) wakimkabidhi mkurugenzi wa kampuni ya Super Terrazzo Ltd Nish Hiran tuzo baada ya kuibuka mshindi wa usambazaji wa bidhaa za kampuni hiyo katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam .
Kampuni inayojishughulisha na utengenezaji wa vifaa vya
ujenzi ya Knauf Gypsum Tanzania imesema mazingira ya uwekezaji hapa nchini
yameboreka kwa kiasi kikubwa na kutangaza kuwekeza shilingi bilioni 115 katika
upanuzi wa kiwanda chake kilichopo Mkuranga mkoani Pwani.
Kampuni hiyo yenye asili ya Ujerumani tayari
imeshawekeza kiasi cha shilingi bilioni 163 hapa nchini kwenye kiwanda na
uzalishaji wa vifaa mbali mbali vya ujenzi wa nyumba ikiwamo gypsum na imesema
itawekeza kiasi kingine cha shilingi bilioni 115 kufikia mwaka 2025.
Akizungumza wakati wa halfa ya chakula cha jioni
kilichoandaliwa kwa ajili ya kuwashukuru wateja wake na wadau mbalimbali,
Mkurugenzi wa Knauf ukanda wa Afrika Mashariki Ilse Boshoff ameishukuru
serikali, wateja na wadau mbali mbali kwa kuifanya safari ya uwekezaji wa
kampuni hiyo hapa Tanzania yenye mafanikio.
“Kila kunapokucha kampuni ya Knauf inapiga hatua
kadhaa mbele. Historia yetu kwa hapa Tanzania ilianza mwaka 2014 tulipofungua
ofisi na baadaye kuanzisha Kampuni ya Knauf Gypsum Tanzania na kuanza kazi
rasmi mwaka 2017,” alisema.
Mkurugenzi huyo alifafanua kuwa mwaka 2018 kampuni
hiyo ilianza ujenzi wa kiwanda cha kisasa kilichopo Mkuranga mkoani Pwani na
mwaka 2020 kilianza uzalishaji kikiwa na uwezo wa kuzalisha mita za mraba
milioni 15 kwa mwaka.
Akitangaza uwekezaji zaidi katika kiwanda hicho
alisema.,“Uwezo wa uzalishaji kwa kiwanda cha Mkuranga ni mita za mraba milioni
15 kwa mwaka na malengo yetu ni kukipanua na kukiwezesha kuzalisha mita za
mraba milioni 43 kwa mwaka kufikia mwaka 2025. Uwekezaji huu utagharimu
shilingi bilioni 115,”